Taarifa ya Ofisi ya Makamu wa Rais kuhusu taasisi ya Samia Habari Suluhu
Ofisi
ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakanusha taarifa
inayosambaa katika Mitandao ya Kijamii kuhusu Taasisi ya Kiraia
ijulikanayo kama Samia Habari Suluhu.
Taasisi
hiyo inajitambulisha kuwa inatoa mikopo ya fedha taslim, pikipiki na
bajaji kwa wanawake wajasiriamali kwa masharti ya kuweka dhamana ya
fedha taslimu shilingi laki mbili.
Ofisi inapenda kuujulisha umma kuwa taarifa hizo ni za uongo na uzushi na zina lengo la kuupotosha umma wa Watanzania.
Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu
Hassan, hamiliki taasisi yoyote ya aina hiyo na hahusiki kwa namna
yoyote na kazi za taasisi hiyo na wala haitambui taasisi hiyo.
Ofisi
ya Makamu wa Rais inawataka Wananchi kuzipuuza taarifa hizo
zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii kwani zinalenga kuleta taharuki
na kupotosha Umma wa Watanzania.
Imetolewa na:
Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ikulu- Dar es Salaam
