MTENDAJI ATUMIA TANGAZO LA SERIKALI KUOMBA RUSHWA.



Na COSTANTINE MATHIAS, Simiyu.

MTENDAJI wa Mtaa Mondo kata ya Guduwi, halmashauri ya mji wa Bariadi mkoani Simiyu amejikusanyia zaidi ya shilingi 300,000/= kwa njia ya udanganyifu kupitia Tangazo la serikali liliowataka vijana waliohitimu kidato cha nne kuomba  nafasi za uhudumu wa afya ngazi ya vijiji.

Kufuatia Tangazo toka wizara ya afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto wametangaza nafasi za masomo ya uhudumu wa afya ngazi ya jamii kwa mwaka 2017/18 likiwataka vijana waliohitmu kidato cha nne na ufaulu wa masomo 4 kwa wastani wa D huku somo la Biology likipewa kipaumbele.

Inadaiwa kuwa Mtendaji huyo Fred Joseph amekuwa akiwatoza fedha vijana hao ili kuwasaidia juu ya kufanya maombi ya nafasi hizo wakati tangazo liliwataka kulipia elfu 30,000/= kwa ajili ya udahili wa Nacte.

Wakiongea kwa nyakati tofauti na waandishi wa Habari vijana hao walisema kuwa baada ya kusomewa Tangazo hilo na sifa zake, walipomfuata mtendaji kwa ajili ya kuwaidhinisha anawaomba fedha akidai kuwa atawasadia kutuma maombi yao na kuhakikisha wanapata nafasi.

‘’kila aliyekidhi sifa za uombaji akienda kwa mtendaji anaombwa fedha…akikosea haidhinishiwi, hivyo kulingana na hali tuliyonayo tunawaomba wazazi fedha na kumpa tukijua ni maelekezo toka wizara ya afya’’ alisema mmoja wa Vijana ambaye jina linahifadhiwa.

Aliongeza kuwa kuna vijana wawili kila mmoja ametoa laki mojamoja, wengine wawili na yeye akiwemo wametoa shilingi elfu 50,000/= kila mmoja na kijana mmoja ametoa shilingi elfu 30,000/=.

Mratibu wa zoezi hilo toka kituo cha Afya Muungano Yustina Sweya alisema kuwa baada ya kupokea Tangazo hilo toka Wizarani walilipeleka kwa wananchi kama lilivyo ili atakayekidhi vigezo atume maombi kwa gharama ya shilingi elfu 30 tu.

Aliongeza kuwa mtedaji huyo anafanya makosa kuwaomba fedha vijana hao kwa ajili ya kuwaidhinisha kwa kuwa hayo ni moja ya majukumu yake na wao hawajaaagiza kutoza vijana hao fedha yoyote.

Mganga Mfawidhi wa Halmashauri ya mji wa Bariadi Akilimali Mpozemenya alisema kuwa kufuatia Tangazo hilo hawajaagiza vijana kutozwa fedha na kuhakikisha kuwa watamkata mtendaji huyo anayeidharirisha wizara kwa kuwa haikutoa maelekezo kama hayo.

‘’hii ni fedheha kwa wizara ya afya inayofanywa na baadhi ya watumishi katika maeneo yao sisi hatujaagiza kufanyika, nadhani tangazo linajitosheleza katika maelekezo yake…hivyo tutahakikisha mtendaji huyo anakamatwa kwa sababu anawaibia vijana wetu’’ alisema Mpozemenya.

Kwa upande wake  Fred Joseph alisema kuwa yeye ni mtendaji wa mtaa wa Mondo na amekuwa akikaimu mtaa wa Guduwi mbugani hivyo hajawahi kuomba fedha na badala yake wajumbe wa serikali ya mtaa wakati wa kupitisha majina hayo wanawaomba fedha ya maji kwa vijana hao kwa sasabu wamepata nafasi hizo bure.

Aliongeza kuwa hadi sasa wamepitisha vijana wanane na yeye kama kiongozi hahusiki na kuongeza kuwa wajumbe wake ndiyo wamekuwa wakiwaomba fedha vijana hao na yeye akipatia kidogo kutokana na kufanya uhamasishaji ili wajitokeze kwa wingi.

‘’mondo kuna vjiana wanne, mbugani wapo wanne, nafanya uhamasishaji ili vijana wajitokeze kwa wingi, nawaandikia barua ya kuwaidhinisha, nawaandikia muhtasari karatasi tano pia naambatanisha na vivuli vya vyeti vyao ili kuwasaidia…mimi sijawahi kuwaomba fedha isipokuwa wajumbe wangu wanaomba pindi tunapokuwa tunapitisha majina’’ alisema Fred.

Alisema kuwa hata yeye ameshasikia tuhuma hizo juu ya vijana hao kutozwa fedha, lakini amekuwa wakiwashauri wajumbe wake wasiwatoze kiwango kikubwa cha fedha kisichozidi elfu 50,000/= ili 30,000/= itumike kufanya maombi na inayobaki wagawane.
Wizara ya afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia ofisi ya Mganga mkuu wa Halmashauri ya mji wa Bariadi imetangazia nafasi za masomo ya uhudumu wa afya ngazi ya vijiji kwa vijana waliohitumu kidato cha nne au cha sita ili baada ya kuhitimu mafunzo hayo waweze kutoa huduma kwa wananchi katika maeneo ya vijijini na kupunguza changamoto ya uhaba wa watumishi wizara ya afya.





Powered by Blogger.