Waziri Mkuu: Akiba ya Fedha za Kigeni Imeongezeka na Kufikia dola 5.91 bilioni za Marekani
Waziri
 Mkuu Kassim Majaliwa amesema akiba ya fedha za kigeni imeongezeka na 
kufikia dola 5.91 bilioni za Marekani kiwango ambacho hakijawahi 
kufikiwa kwa takriban miaka minne kuanzia mwaka 2013 hadi 2016.
Ameyasema
 hayo leo Februari 9, 2018  bungeni mjini Dodoma wakati akitoa hoja ya 
kuahirisha mkutano wa 10 wa Bunge la 11. Bunge limeahirishwa hadi Aprili
 3, mwaka huu.
Amesema
 mbali na kuongezeka kwa akiba ya fedha za kigeni, pia thamani ya mauzo 
ya bidhaa na huduma nje ya nchi imekuwa takriban dola 8.695 bilioni za 
Marekani ikilinganishwa na wastani wa dola 8.828 bilioni za Marekani kwa
 miaka mitatu iliyopita.
Hata
 hivyo, amesema utekelezaji wa bajeti kwa kipindi cha nusu mwaka ni wa 
kuridhisha ambapo ukusanyaji wa mapato ulifikia Sh12.95trilioni sawa na 
asilimia 82.8 ya lengo lililopangwa katika kipindi hicho.
Amesema
 matumizi ya fedha hizo yameelekezwa katika kugharamia shughuli 
mbalimbali za Serikali za kuhudumia wananchi na miradi ya kipaumbele 
ambayo ni kuanza kwa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa.
Pia
 kugharamia mpango wa elimumsingi bila malipo, kugharamia mpango wa 
ununuzi wa dawa, vifaatiba na vitendanishi na utekelezaji wa miradi ya 
usambazaji maji vijijini na mijini na usambazaji wa umeme vijijini 
kupitia REA. 
Miradi
 mingine ni ununuzi wa meli za abiria na mizigo katika maziwa, ukarabati
 na ujenzi wa baadhi ya viwanja vya ndege na kujenga na kuendeleza 
maeneo ya uwekezaji wa viwanda katika mikoa mbalimbali nchini.
“Hakika
 kwa mafanikio haya tuna kila sababu ya kumpongeza Rais John Magufuli 
kwa uongozi wake mahiri na juhudi anazofanya za kuhakikisha kuwa 
wananchi wanapata huduma muhimu na maendeleo ya haraka,” amesema.
Waziri
 Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha kuwa inatekeleza 
ahadi zake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba malengo yaliyowekwa kwa
 mwaka 2017/2018 yanafikiwa kwa kiwango kikubwa.
Amesema
 kuwa Serikali itaendelea kuimarisha na kujenga misingi na mifumo imara 
ya ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa lengo la kuwa na mapato endelevu 
kwa ajili ya kugharamia matumizi yake.
Vilevile,
 kuwa na usimamizi madhubuti wa ukusanyaji wa mapato ambao utasaidia 
kupanua wigo na kudhibiti ukwepaji wa kodi kupitia urasimishaji wa 
shughuli za uchumi kwa kuwezesha ukuaji wa biashara katika sekta ndogo 
na za kati ambazo ndiyo mihimili ya kuzalisha ajira na kukuza uchumi.
Akizungumzia
 kuhusu viashiria mbalimbali vya kiuchumi, Waziri Mkuu amesema 
vinaonyesha kwamba hali ya uchumi ni nzuri na pato la Taifa katika 
kipindi cha Julai hadi Desemba, 2017 lilikua kwa wastani wa asilimia 
6.8.
“Hali
 hii inaashiria kwamba tuna matarajio makubwa ya kufikia lengo la mwaka 
la ukuaji wa asilimia 7.0. Sekta zilizochangia kwa kiwango kikubwa 
katika ukuaji huo ni habari na mawasiliano, uchimbaji madini, biashara, 
ujenzi na uzalishaji viwandani,” amesema.
