Serikali Yafanikiwa Kurejesha Mali Za NCU, SHIRECU
WAZIRI
 MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imefanikiwa kurejesha mali tisa 
kati ya 10 za Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU) ambazo 
zilichukuliwa kinyume cha taratibu na kuagiza watuhumiwa wachukuliwe 
hatua za kisheria.
Amesema
 mali moja iliyobakia bado inafanyiwa uchunguzi na mali mbili za Chama 
Kikuu cha Ushirika cha Shinyanga (SHIRECU) nazo pia zimepatikana lakini 
bado ziko kwenye hatua ya makabidhiano.
Waziri
 Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Februari 9, 2018) bungeni mjini 
Dodoma wakati akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa 10 wa Bunge la 11. 
Bunge limeahirishwa hadi Aprili 3, mwaka huu.
Waziri
 Mkuu amezitaja mali za Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU) 
zilizorejeshwa kuwa jengo la Nyanza Cooperative Union (1984) Ltd. 
maarufu kwa jina la “Transport House” au KAUMA House, lililopo katika 
kiwanja namba 242, Kitalu T, Mtaa wa Stesheni; kiwanda cha kusindika 
mafuta cha New Era Oil Mill, kilichopo katika eneo la Igogo; na jengo na
 viwanja vya Ashock Industries vilivyopo eneo la viwanda Igogo.
Nyingine
 ni majengo ya kilichokuwa kiwanda cha mkonge na dengu kilichopo eneo la
 Igogo kwenye kiwanja namba 41 na 79; jengo lililopo katika kiwanja 
kilichopo Isamilo namba 80, kitalu “D”; jengo lililopo katika kiwanja 
kilichopo Isamilo namba 110, kitalu “D” na ghala moja katika kiwanja 
namba 104, kitalu “A” kilichopo eneo la Igogo.
“Mali
 nyingine zilizorejeshwa ni jengo moja lililopo mjini Geita katika 
kiwanja namba 8 Kitalu “K”; jengo moja lililopo mjini Geita, katika 
kiwanja namba 24, Kitalu “K” na jengo lililopo Isamilo katika kiwanja 
namba 89 Kitalu “D”,” amesema Waziri Mkuu.
Kwa
 upande wa mali za SHIRECU, Waziri Mkuu amezitaja mali zilizopo kwenye 
hatua ya makabidhiano kuwa ni ghala lililopo Kurasini, Dar es Salaam na 
nyumba ya ghorofa tatu iliyopo kiwanja namba 1001 “BB” Ilala, jijini Dar
 es Salaam.
“Katika
 kusimamia misingi ya utawala bora na uwajibikaji wa watendaji wa vyama 
vya ushirika, Serikali inaendelea kufanya uchunguzi maalum kuhusu 
mikataba mibovu ya Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU), Chama 
Kikuu cha Ushirika cha Shinyanga (SHIRECU), Chama Kikuu cha Ushirika cha
 Kagera (KCU) na Chama Kikuu cha Ushirika cha Kilimanjaro (KNCU). 
Vilevile, tunachunguza kushikiliwa kwa mali za ushirika bila kufuata 
utaratibu,” amesema.
Amesema
 Serikali itaendelea kuviamsha vyama vya ushirika vya msingi na vyama 
vikuu vilivyosinzia katika mikoa yote ili kujenga ushirika imara na 
kwamba juhudi na hatua hizo zinazochukuliwa na Serikali, zinalenga 
kuongeza imani, hamasa na uzalishaji wa mazao na kusimamia masoko yake, 
na hivyo, kuinua kipato cha wakulima sambamba na kuwapatia fursa ya 
kujiajiri wenyewe katika sekta ya kilimo.
