SIMAMIENI MAENDELEO NA HAKI ZA WATOTO.






                               MEATU:

Wananchi na wakazi wa  Mkoa wa Simiyu wametakiwa kusimamia,  kuimarisha na kuendeleza haki za watoto  ili kila mtoto aliyefikisha umri wa kuanza shule anaandikishwa ili kwenda sambamba na malengo ya millennia.

Akiongea katika maadhimisho ya siku ya mtoto Duniani kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Simiyu Paschal Mabiti, mkuu wa Wilaya ya Bariadi Erasto Sima alisema viongozi simamieni haki za watoto,  ambapo maadhimisho hayo  Mkoa wa Simiyu yalifanyika katika Uwanja wa stendi ya mabasi Wilaya ya Meatu.

Sima alisema kuwa haki ya mtoto ni mahitaji yote muhimu yaliyo ya  lazima na anayopaswa kupatiwa mtoto ili kumjengea msingi mzuri na bora wa maisha yake ya baadae atakapokuwa mtu mzima ili awe mwenye kulifaa taifa na jamii kwa ujumla.

Alisema kuwa lengo la taifa ni kuhakikisha  kila mtoto anapata elimu bora na kwamba jamii kwa kushirikiana na serikali iweze kuimalisha ujenzi wa madarasa zaidi ili kuruhusu watoto wote wenye umri wa kwenda shule kupata elimu bora.

Sima alisema kuwa pamoja na kuweka msisitizo wa upatikanaji wa haki za watoto mkoani hapa zipo changamoto nyingi ambazo zinachangia kutokuelewa kikamilifu haki za watoto ambao wanaonekana kutengwa na jamii.

Alizitaja changamoto hizo ni pamoja na ukatili wa wazazi/walezi kwa watoto ikiwa ni  kuwapiga au kuwapa adhabu kubwa zisizostahili na umri wao, kuwepo kwa ubaguzi unaotolewa  na wazazi katika kumpatia mtoto haki yake ya elimu.

Changamoto zingine ni mtoto kutumikishwa kazi nyingi na ngumu kulingana na uwezo wake kwa kuchunga mifugo, kulima, kufanya biashara ndogondogo, watoto wengine kutunza familia, kufanya kazi za nyumbani hasa kwa watoto wa kike.

“tusimamie maendeleo na makuzi ya watoto haipendezi kuona jamii kubwa inayotegemewa na taifa ikiwa imepoteza mwelekeo wa maadili mema wakati sisi wazazi bado tungali hai”Alisema Sima

Kwa upande wake Afisa maendeleo ya wilaya ya Meatu Egiekiel Mkuki alisema kuwa licha ya kuwepo na changamoto hizo wanayo mikakati mbalimbali ya kuweza kuwasaidia watoto kupata elimu bora na kuweza kukua katika maadili ya kitanzania.

Mkuki alisema serikali inahakikisha inaunda mabaraza ya watoto pamoja na kamati za halmashauri ambazo zitakuwa zinasimamia matatizo ya watoto katika wilaya  na kutatua matatizo ya watoto ambayo yatajitokeza ili kuweka mazingira mazuri ya watoto kuweza kusoma na kupata elimu bora.

MWISHOTop of Form
Bottom of Form
Powered by Blogger.