Milioni 1 adhabu ya ufugaji mifugo holela Mjini


Na James Timber, Mwanza
Ufugaji mifugo holela ni kosa la jinai katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela ambapo kima cha chini cha adhabu iwapo utakutwa na kosa hilo ni shilingi milioni moja au kutumikia kifungo cha miezi sita jela.

Hayo yamesemwa katika Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela John Wanga kwa niaba ya Mgeni Rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella, ambapo kiwilaya yamefanyika Kata ya Kawekamo na kuwataka wananchi kusimamia na kuitunza miti iliyopandwa kutoka eneo la Kona ya Malaika mpaka Misheni Makongoro.

"Tumepanda miti ya miembe pembezoni mwa barabara kuu ya Uwanja wa ndege naomba wananchi wazingatie utunzaji wa mazingira, ukihitaji kukata mti lazima uwe na kibari. Ujenzi holela haurusiwi kwani ni chanzo cha uharibifu wa mazingira pia lazima upate kibari kabla hujajenga kutoka Idara ya mpango Mji," alisema Wanga.

Wanga alieleza kaulimbiu ya Maadhimisho hayo kuwa ni "Mkaa ni gharama tumia nishati mbadala" ambapo amewaomba wananchi kutumia nishati ya gesi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani badala ya matumizi ya mkaa kwani yana gharama kubwa.

Kwa upande wake Afisa Mazingira katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela Simon Nzagi alisema kuwa lengo la kupanda miti ya miembe ni kuweka kivuli pembezoni mwa barabara na miti hiyo inatoa matunda pia ni pendekezo la Mkuu wa Mkoa, ambapo lengo ni upandaji wa miti 340 na zoezi hilo litakuwa endelevu.

Aidha Nzagi alitoa wito kwa wananchi kuepuka watu wasikate miti kwa ajili ya utengenezaji wa mkaa kwani wanasababisha ukame katika nchi sambamba na vifo vya wanyama kwani maji na vyakula vitapungua.
Powered by Blogger.