MGOMBEA URAIS RAILA ODINGA APINGA MATOKEO YA UCHAGUZI YANAYOTANGAZWA NA TUME YA UCHAGUZI IEBC
Mgombea urais wa muungano wa upinzani nchini Kenya National Super
Alliance (Nasa) Raila Odinga amepinga matokeo ambayo yanaendelea
kutangazwa na tume ya uchaguzi nchini humo, IEBC.
Bw Odinga amewaambia wanahabari kwamba tume hiyo imekuwa ikitangaza matokeo kwenye tovuti yake na kufuata utaratibu ufaao.
Waziri mkuu huyo wa zamani amesema kabla ya matokeo yoyote kutangazwa,
IEBC inafaa kuwapa maajenti wa vyama Fomu 34A kutoka vituoni.
Amesema kwa sasa, bila kuwepo kwa fomu hizo, ni vigumu kubaini matokeo yanayopeperushwa yanatoka wapi.
"Mfumo umeacha kufanya kazi. Sasa ni mitambo inayopiga kura. IEBC
wamesema kwamba hakuna chama chochote kilichopinga matokeo. Lakini vyama
vitapingaje matokeo bila kujua asili yake? Ni fomu 34A pekee
zinazoonesha chanzo cha matokeo," amesema.
"Kwa hivyo, tunakataa matokeo yote yaliyotangazwa kwa sasa na kuitaka
tume ya IEBC itoe fomu 34A za kila kituo kabla ya matokeo zaidi
kutangazwa."
IEBC imekuwa ikitangaza matokeo ya urais mtandaoni, na kufikia saa tisa
na robo alfajiri, matokeo hayo yalikuwa yanamuonyesha Rais Uhuru
Kenyatta wa chama cha Jubilee akiwa mbele na kura 6331140 (55.27%) naye
Bw Odinga akiwa na kura 5031737 (43.92%).
Matokeo hayo ni ya kutoka vituo 295319 kati ya vituo 40883 nchini humo.
"Hii ni kompyuta inayopiga kura," alisema Bw Odinga akikataa matokeo hayo.
Hali ya wasiwasi imekuwa ikitanda katika kituo cha taifa cha kujumlishia
na kutangaza matokeo katika ukumbi wa Bomas jijini Nairobi.
Matokeo yalianza kutiririka baadaye Jumanne jioni baada ya shughuli ya
kuhesabiwa kura kuanza. Matokeo hayo yamekuwa yakionesha Bw Kenyatta
akiongoza.
Wakala mkuu wa muungano huo wa upinzani, naibu waziri mkuu wa zamani
Musalia Mudavadi alikuwa awali amehutubia wanahabari na kutaja matokeo
yanayotangazwa na tume hiyo kama utapeli.
Alitoa wito kwa wafuasi wa muungano huo kupuuzilia mbali matokeo yanayotangazwa.